Friday, January 15, 2016

KUMCHA BWANA/THE FEAR OF THE LORD




Kumcha BWANA ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu” (Mithali 1:7).

The fear of the Lord is the beginning of knowledge; fools despise wisdom and instruction” (Prov. 1:7 ESV).

Kuna jambo zuri la kujifunza hapa leo. Nitatumia mfano. Wakati wa vita kuna mambo mawili yanaweza kusababisha ushindi. Jambo la kwanza ni SILAHA na jamabo la pili ni MBINU za vita.

Siku zote ushindi wa vita hautegemei UBORA wa silaha peke yake. Na kwa upande mwingine, UTENDAJI wa silaha hautegemei mtu anayetumia ila NGUVU iliyoko nyuma ya huyo MTU. Kwa mfano, Goliath alikuwa na SILAHA bora na kali kuliko Daudi, pia Goliath alikuwa Jemadari na mzoefu wa vita. Tofauti ya Goliath na Daudi ilikuwa (1). Nguvu iliyokuwa nyuma yao, na (2). Maarifa katika Mungu (Knowledge of God).

Siku zote Daudi akisikia Vita, alikuwa anasema “hawa wanataja magari na farasi (silaha), ila mimi nitalitaja Jina la Bwana”. Sasa usidhani Daudi alikuwa habebi upanga, Daudi alikuwa anabeba upanga kama wenzake, ila HAKUUTEGEMEA upanga wake. Alijua siri ya USHINDIni katika mambo mawili: Kumjua Mungu wake na Nguvu za Mungu wake.

Hebu tuangalie kumcha Mungu ni kitu gani. Ukitaka kujua kipimo cha UCHA MUNGU wako, zingatia hapa, “the fear of the Lord”. Jiulize, ni kwa kiwango gani “una hofu ya Mungu” ndani yako? Yesu alipokuja, hakutaka kupingana na Torati, na wala hapingani nayo, ila ilitaka watu wamjue BABA kwa namna ya tafauti na  walivyomjua mwanzo. Hebu angalia hapa, “Mmoja wao, mwana-sheria, akamwuliza, akimjaribu; Mwalimu, katika torati ni amri ipi iliyo kuu? Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii(Mat. 22:35-40).

 Kuna tofauti ya HOFU ambayo imejikita katika “UPENDO” na HOFU iliyojikita katika “HUKUMU”. Ukiona HOFU inayokufanya usifanye “JAMBO” fulani lolote inatokana na kuogopa HUKUMU, yaani lawama, adhabu, kushangaliwa, sheria ya nchi, nk., hiyo SIO hofu ya Mungu ila ni HOFU ya HUKUMU. Watu wengi wameenenda kwa namna fulani kwa kuogopa (kuwa na hofu ya wanadamu)  JAMII inayowazunguka, na wala sio Mungu wao! Mchamungu siku zote kinachomsukuma kutofanya jambo, au kufanya kitu, ni UPENDO kwa Mungu wake.HOFU ya kumtenda Mungu dhambi, au KIU ya kumpendeza Mungu ndio inayomsukuma kufanya jambo fulani au kuacha kufanya jingine. Mtu wa namna hii anaitwa “mchamungu”.

Hebu angalia tena hapa, Yesu “Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza.” Hii ni AMRI kuu. Ukifika mahali pa KUMPENDA Mungu kwa moyo wako wote (katika kuwaza kwako), roho yako yote (uhai wako sio kitu kuliko kumkosea Mungu wako), akili zako zote (maamuzi yako, matendo yako, nk.), hii ni hali ya JUU kabisa ya KUMCHA Mungu. Angalia tena, “Mpende Bwana Mungu wako”, kinachokusukuma ni“UPENDO” sio “HUKUMU”.  Zingatia hapa “Bwana Mungu WAKO”, sio “WENU”. Ikifika mahali pa mtu na Mungu, hakuna “ujumla”, ni wewe na “Mungu wako”. Kila mtu atasimama kama yeye na sio “nyie”. Ndio maana unatahadharishwa “angalia mtu asijekuitwaa taji yako”. Taji “yako”, utaipigania wewe mwenyewe na sio kiongozi wako kanisani, wala mzazi au mke/mume, ni wewe na Mungu.

Kuna tofauti ya mtu anayempenda Mungu kwa sababu anampenda Mungu, na mwingine anampenda Mungu kwa hofu ya JEHANAM. Anayempenda Mungu kwa sababu anampenda Mungu huangalia kumpendeza Mungu bila kutarajia “malipo”, any form of reward. Yaani hawezi kufika mahali akalinganisha kuanguka, kushindwa, majanga, nk., na MUNGU kuwa kinyume chake. Anayempenda Mungu kwa kuogopa JEHANAM, siku zote utamsikia akiwa busy na kutumia NGUVU kupambana na dhambi. Na kwa sababu yuko busy kupambana na dhambi, katika maisha yake DHAMBI ni dhahiri kuliko UTAKATIFU. Ndio maana utamwona siku zote anahesabu na kushangaa dhambi za watu wengine na kujihesabia haki tu. Mtu anayempenda Mungu kwa sababu anampenda Mungu, dhambi sio option katika maisha yake kwamba afanye au asifanye, moyoni mwake hana uchaguzi kwa maana hatamani hiyo dhambi. Huwezi kupambana na kitu usichokitamani. Ukimpenda Mungu sana, moja kwa moja unajikuta unakuwa MSHINDI, na ukisikia mtu ameanguka dhambini, inakuuma kama vile wewe ndio umeanguka, na ule UPENDO utakusukuma kuwaombea wengine na sio kuwasengenya na kuwasema tu.

Hebu angalia hapa, “atendaye dhambi ni wa Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu mwanzo. Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi. Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu. Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake.” (1Yoh. 3:8-10). Dunia imewafikisha watu mahali pa kusahau kwamba Mungu ni Mtakatifu sana, hofu imegeuka kuwa “hofu ya dhambi (hukumu)” na wala sio “hofu ya Mungu”. Paulo alifika mahali akasema “sheria inawahusu wakosaji”, yaani kama wewe ni “mwana wa Mungu”, sheria ya “usizini”, “usiibe”, nk., haikuhusu kwa sababu , huna “kiu” na hiyo dhambi. Ukiangalia hapo katika 1Yohana 3:8-10, utaona Yohana pia amesisitiza UPENDO. Msingi wa hili fundisho la Yohana ni KUMPENDA Mungu na ndugu yako (watu wengine).

Angalia hapa, “Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni. Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake” (Ayubu 2:8-10). Mtazamo ya mke wa Ayubu ulikuwa, kufanikiwa ndio “nguvu” ya kumcha Bwana. Ayubu alijua kwamba “hakuna uhusiano kati ya majaribu, magumu, shida, nk, na UTIMILIFU au UCHA MUNGU wake”, katika shida na raha, alimheshimu Mungu kiasi cha kupata shida hata akifikiri tu kwamba “labda” watoto wake wanatenda dhambi huko, licha ya yeye mwenyewe, na ilimpasa “atoe sadaka” kwa ajili yao, ili Mungu awarehemu tu, japo hana uhakika kama wanatenda dhambi au la. Huu upendo hauwezi kukuruhusu UKAMSENGENYA ndugu yako aliyeanguka dhambini, utasimama na kuomba rehema ili Mungu amtegemeze asianguke tena. Hii ni moja wapo ya sifa za wachamungu, kutegemezana na sio kuangushana au kuchekana kwenye kushindwa.

Nikirudi katika kumchamungu, faida zake ni nyingi. Moja wapo niudhihirisho wa Mungu maishani mwako. Jinsi unavyozidi kumcha Mungu, na kumpendeza, ndivyo utazidi kumwona, na HOFU ya Mungu itaongezeka. Angalia tena hapa “Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema, Kweli BWANA yupo mahali hapa, wala mimi sikujua. Naye akaogopa akasema, Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka, hapa ni nyumba ya Mungu, napo ndipo lango la mbinguni” (Mwa. 28:16-17). Baada ya Yakobo kupokea baraka, na kuwatii wazazi wake (kwa sababu hakuoa Wakanani (wamataifa) kama Esau ndugu yake), Mungu aliendelea kumbariki na kujidhihirisha kwake. Angalia tena hapa, “Kweli BWANA yupo mahali hapa, wala mimi sikujua”! Yakobo anashangaa kwamba “kumbe” Mungu yuko hapa na hakujua. Angalia tena hapa, Mahali hapa panatisha kama nini!”hofu ya Mungu ilishuka juu yake zaidi kuliko mwanzo, na ukisoma mistari inayofuata akasukumwa na kutoa SADAKA (fungu la kumi la mali zake) pia. Hofu ya Mungu ambayo Msingi wake ni Upendo KWA Mungu, itakusukuma kumtii Mungu, kwa sababu unamwogopa Mungu na sio kwa sababu unaogopa Dhambi au HUKUMU. Na hii ndio maana ya kuwa mchamungu.

Mungu akubariki sana, endelea kuwa nasi kwa makala mbalimbali.